EWE MJASIRIAMALI, HATUA ZA KUUNDA KAMPUNI HIZI HAPA, MILIKI KAMPUNI SASA.
Na MTAALAMU WAKO
STEP 1; chagua jina.
Kampuni lazima iwe na jina linalotambulika na linalojitofautisha na majina ya makampuni mengine nchini.
Hatua hii, kwa lugha ya biashara huitwa ‘Name Search’ ambapo unatakiwa kutumia online account ya Brela kuuliza iwapo jina ulilochagua linafaa na hakuna linapotumika Tanzania.
Jina hilo litaingizwa kwenye mtandao wa makampuni yaliyosajiliwa na Brela, ili kuona kama kuna kampuni yenye jina linalofanana na hilo lako.
Kwa kuwa majina yote ya kampuni nchini yako ofisi hiyo, hivyo si rahisi kampuni zaidi ya moja kuwa na majina yanayofanana. Ikibainika kuwepo kwa kampuni yenye jina kama la kwako,
Ofisa wa Brela, atakuelekeza utafute jina jingine, na kama atakuta hakuna jina la kampuni linalofanana na la kwako, basi jina hilo litapokelewa kwa hatua inayofuata.
STEP 2; andaa waraka na katiba ya kampuni (memorundum&article of association).
Baada ya jina kuwa limethibitishwa, kwa maana ya kukubaliwa na Msajili wa Kampuni, hatua inayofuata ni kuwasilisha kwa Msajili waraka wa kampuni na katiba ya kampuni.
Waraka wa kampuni au kwa lugha ya kigeni ‘memorandum of association’, ni waraka maalum uliosainiwa na wanachama wote ambao hueleza na kuchambua kile ambacho kampuni itakifanya.
Shughuli zinazotarajiwa kufanywa na kampuni zinatakiwa kuelezwa vyema ndani ya waraka huu. Waraka huu lazima uwe na mhuri wa mwanasheria.
Katiba ya kampuni au kwa lugha ya kigeni, ‘article of association’ kwa upande mwingine, nayo lazima iwe imesainiwa na wanachama wa kampuni husika. Katiba hii ndiyo inayoeleza uendesahaji mzima wa kampuni.
Aidha, inaeleza haki na wajibu wa wanahisa, uongozi wa kampuni, mgao wa mapato, nguvu na mamlaka ya wakurugenzi, mikutano na utaratibu wake, umiliki na ugawaji wa hisa, uhamisho wa hisa na kadhalika. Hii nayo lazima iwe imesainiwa na mwanasheria.
Wanahisa na wanachama wa kampuni watasaini katika nyaraka hizi zote mbili. Nyaraka hizi huwekwa katika mfumo wa vitabu na hutakiwa kuanzia vitabu vinne.
STEP 3 ; jaza fomu 14a&14b.
Baada ya kusaini hapo juu, basi ijazwe fomu maalum yenye maelezo yanayohusu anuani kamili ya ofisi za kampuni. Anuani hapa si tu Sanduku la Posta, bali pia mahali zilipo ofisi za kampuni, kwa maana ya mahali ambapo kampuni hiyo itaendeshea shughuli zake.
Pia itajazwa sehemu ya wasifu wa wakurugenzi wa kampuni pamoja katibu wa kampuni.
Aidha, lazima ijazwe fomu maalum ambayo ipo kama kiapo kuonesha kuwa matakwa yote ya kisheria yametimizwa, hivyo kampuni inatakiwa kupatiwa usajili.
Fomu hiyo itajazwa na mmoja wa wakurugenzi wa kampuni na itatiwa mhuri na Wakili.Fomu hii inakuwa ni ushahidi kuwa matakwa yote yametimizwa kwa ukamilifu.
STEP 4 ; jaza fomu ya maadili.
Hii ni fomu mpya haikuwepo hapo nyuma. Inatakiwa kujazwa na mmoja wa wakurugenzi wa kampuni.
STEP 5 ; peleka nyaraka zote Brela (filing).
Utabeba vitabu vya waraka na katiba ya kampuni, utabeba fomu ya maadili na ile ya wasifu utapekeka Brela. Hapo watakagua ikiwa ziko sawa utafanyiwa makadirio ili ukalipe.
STEP 6 ; malipo ya ada.
Zipo aina tatu za ada ambazo ni registration fee, filing fee, na stamp duty.
Kampuni italipa ada kutokana na ukubwa wa mtaji wake. Mathalan kampuni ya mtaji wa m1- m5 ada zote tatu ni kama 167,000/= hivi, ya mtaji wa m5- m10 ada zote tatu ni kama 267,000/= hivi, ya mtaji wa m10-30 ada zote tatu kama 467,000/= ya mtaji wa m30- m50 ada zote tatu ni kama 567,000/ na mwisho ni ile ya mtaji wa m50- na kuendelea bila ukomo ada zake zote tatu zinafika kama 700,000/= hivi.
Jambo la kuzingatia ni kuwa mtaji uliotajwa hapa huitwa "the proposed capital". Sio fedha halisi ambayo lazima uwe nayo mfukoni.
Maana yake waweza kusajili kampuni ya mtaji wa bilioni 1 huku mfukoni unazo laki mbili. Haikatazwi kwasababu mtaji ulioandikwa ni unapendekezwa tu"proposed" na sio halisi.
Pia, ukubwa wa mtaji wa kampumi haukuongezei malipo ya kodi. Malipo ya kodi hawaangalii mtaji wa kampuni bali vitu vingine.
Juu ya hilo, malipo haya hulipwa mara moja katika maisha yooote ya kampuni. Ukilipa mara moja umemaliza .
STEP 7 ; kufuatilia na kupata cheti.
Baada ya kutimiza matakwa yote haya utaambiwa fuatilia tarehe fulani kuona kama usajili umekamilika.
Ikiwa umekamilika tarehe uliyoambiwa basi kampuni itasajiliwa na utapewa Cheti cha Usajili(certificate of incorporation). Na hapo tunasema kampuni itakuwa imezaliwa na kuwa sasa unamiliki kampuni.
NASAHA.
NIshauri kuwa kufanya biashara kwa mfumo wa kampuni, ni muhimu mno kuliko ambavyo baadhi ya watu wanaweza kufikiria.
Karibu biashara zote za kisasa, hufanyika kwa mfumo huo wa kampuni. Asikudanganye mtu kuwa atapatikana mfanyabiashara mkubwa kutoka Ulaya, Amerika au hata hapa kwete ambaye atakubali kufanya biashara na mtu binafsi. Labda biashara hiyo iwe ya kukufanya wewe kuwa kibarua!
Kampuni zote za ndani na nje, huwa hazifanyi biashara na watu binafsi, bali kama kama watu hao wamejiunga pamoja na kuwa kampuni.
Nieleweke vyema hapa kwamba ninaposema biashara, simaanishi biashara kubwa sana, bali biashara hiyo hiyo ndogo unayoifanya, hata kama ni ya ufugaji kuku wa mayai au wa nyama, biashara ya kuuza maziwa biashara ya duka la vyakula, biashara ya huduma ya pesa kwa njia ya simu, kuuza mazao, kijiwe chako cha ufundi magari au seremala na kadhalika, zote hizo usizifanye wewe kama wewe.
Ukweli ni kwamba hakuna atakayekupa kazi ya maana kama wewe ni mtu binafsi. Biashara ya sasa haifanywi hivyo. Usikwamishe kukua kwa biashara zako, anza sasa kuunda kampuni yako!
Comments
Post a Comment